01/06/2026
THE POPULAR INSPIRNG AND RELIEF ORGANIZATION (PIRO) YAONGOZA ZOEZI LA UPANDAJI MITI KUELEKEA MAADHIMISHO YA SIKU YA MAZINGIRA DUNIANI 2026
Katika kuelekea Maadhimisho ya Siku ya Mazingira Duniani yanayoadhimishwa kila tarehe 5 Juni, Taasisi ya The Popular Inspiring and Relief Organization (PIRO) leo imeungana na Wananchi, wanafunzi na wadau mbalimbali katika Bwawa la Kisongoni, Mkoa wa Kaskazini Unguja, kufanya zoezi kubwa la upandaji miti kwa lengo la kuendeleza Zanzibar ya Kijani na kulinda mazingira yetu.
Katika shughuli hiyo, PIRO imefanikiwa kupanda miti zaidi ya 15,000 ya aina mbalimbali ikiwemo Mivinje, Mikungu, Mitondoo, Mianzi, Jakaranda, Mikristimasi, Cedrela na Pongamia. Zoezi hili limeambatana na utoaji wa elimu ya mazingira kwa jamii na wanafunzi ili kuongeza uelewa kuhusu umuhimu wa uhifadhi wa mazingira na vyanzo vya maji.
"Mazingira ndiyo maisha yetu."
Kupanda miti ni hatua muhimu katika kuimarisha uoto wa asili, kuhifadhi vyanzo vya maji, kupunguza athari za mabadiliko ya tabianchi, kuboresha ubora wa hewa na kutengeneza makazi salama kwa viumbe hai.
Akizungumza katika hafla hiyo, Mkurugenzi Kanda wa PIRO alisema:
"Katika kuadhimisha World Environment Day, tunawakumbusha wananchi wote kuwa mazingira si jambo la hiari bali ni msingi wa uhai wetu. Dunia inakabiliwa na changamoto za mabadiliko ya tabianchi, uchafuzi wa mazingira na uharibifu wa misitu. Hatuwezi kubaki watazamaji; kila mmoja ana wajibu wa kuchukua hatua kwa kupanda miti, kupunguza matumizi ya plastiki na kuelimisha jamii kuhusu umuhimu wa kulinda mazingira."
Aliongeza kuwa vijana wanapaswa kuwa mstari wa mbele katika kuleta mabadiliko chanya kwa kutumia ubunifu, maarifa na mshik**ano katika kulinda mazingira kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho.
Tukilinda mazingira leo, tunahakikisha kesho yenye usalama, afya njema na maendeleo endelevu kwa vizazi vijavyo.
PIRO inaendelea kutoa wito kwa wananchi wote kushiriki kikamilifu katika juhudi za uhifadhi wa mazingira kwa kupanda miti, kulinda vyanzo vya maji na kuacha vitendo vinavyoharibu mazingira.
"Hakuna sayari nyingine ya kukimbilia; tuna wajibu wa kuitunza dunia tuliyonayo."