03/06/2025
KALAMU YANGU, RAI YANGU!
HIVI, KAPTURA ZAKO ZOTE NI ZAKO KWELI NA ZINAKUENEA VIZURI MPENDWA!
Wapendwa wasomaji wa makala zangu hamjambo? Mimi sijambo na niko tayari kwa safari yetu ya kutafakari kuhusu maisha. Mlinifurahisha kwa mrejesho wenu wa makala ya wiki jana ambayo ilimuuliza kila mmoja k**a ana salio kwenye bima yake ya kijamii. Endeleeni kusoma makala zangu ili niendelee kupata sababu za kuandika tena na tena.
Wiki hii ninaomba tutafakari kuhusu kaptura zetu. Kila mmoja ana kaptura yake. Hapa ninajua ushaanza kuwaza kaptura! K**a ni mwanamke ushaanza kujiweka pembeni ukijenga hoja kwamba kaptura ni za wanaume! Ni sawa, lakini kaptura ya makala yangu kila mmoja anayo na anaivaa. Unabisha! Funga mkanda tusafiri uone mwenyewe.
Kusema ukweli, uandishi ni raha. Tena, raha inakolea zaidi pale unapopata mrejesho wa wasomaji wako. Makala ya wiki iliyopita ilinipa raha zaidi kutokana na mawazo na unyumbufu wa tafakuri zenu. Mama yangu mmoja ambaye ni Profesa, aliniomba nimtumie makala ile ili asome. Nilipomtumia, mama huyo kwa kweli aliisoma kwa uaminifu. Alipomaliza, alinitumia mrejesho mzuri akisema makala inagusa mambo muhimu ya jamii zetu na akatamani kila mtu aisome. Zaidi, aliniombea nizidi kuandika tena na tena kwa ajili yako wewe unayesoma makala yangu na wengine. Alipomaliza kutoa mrejesho aliniuliza swali, "Lakini mwanangu, haya unayoyaandika huwa unayatoa wapi jamani? Baada ya kutafakari namna ya kumjibu mama, niliona niseme ukweli kwamba mengi ninayoyaandika ninayachota kwenye jamii zetu.
Jibu nililompatia Profesa, lilikuwa la kweli kabisa. Hata mada ya wiki hii nimeitoa kwenye jamii zetu kabisa. Nikiwa ninawaza wiki hii niandike kuhusu nini, nilijikuta ninaijiwa na mambo mengi kichwani. Katika matini zilizokuja kichwani, nilijikuta ninakumbuka mazungumzo kati ya daktari mmoja wa hospitalini na watu waliotaka kujua namna ya kumtibu mtoto mwenye shida ya kuweka kidole kinywani kila mara. Sijui unanielewa hapa!
Daktari alikuwa anaongea na watu ili kubadilishana nao mawazo. Alipoletewa kesi ya namna ya kumsaidia mtoto ambaye anasoma darasa la kwanza, anayetembea muda wote akiwa ameweka kidole cha mkono kinywani, alitoa ushauri ambao uliniacha hoi. Hapo ndipo nilipopata mada ya kuandikia makala ya wiki hii. Daktari alisema kwamba dawa ya mtoto mwenye tabia ya kuweka kidole mdomoni ni ndogo tu. Alisema kuwa mtoto huyo ukimshonea kaptura kubwa inayomzidi kiuno, utakuwa umemsaidia. Mtoto huyo akiwa anatembelea, badala ya kuweka kidole mdomoni, muda wote atatembea akiwa anashikilia kaptura yake na huenda baada ya wiki kadhaa tatizo la kuweka kidole mdomoni likaisha. Badala ya kuweka kidole kinywani, muda wote mtoto atakuwa anapambana na kaptura inayotishia kudondoka. Unaipata picha lakini! Kichwani unaona jinsi mtoto anavyoishikilia kaptura! Unaona anavyohangaika lakini na kusahau kulamba kidole chake?
Nikiwa ninacheka baada ya kukumbuka stori ya Daktari kuhusu matibabu ya mtoto kwa kumshonea li-kaptura li-kubwa, nilijikuta akili inahamia huko Namagondo - Ukerewe, Mwanza nyumbani kwa Prof. E. Kezilahabi. Kwa kweli, nimelazimika kumkumbuka nguli na jabali la fasihi, Prof. Euphrase Kezilahabi ambaye sasa ni marehemu (Hayati!!). Huyu mwamba aliandika sana kazi za kifasihi ambazo zinafikirisha sana.
Tafakuri yangu imezama katika tamthilia yake moja inayoitwa Kaptura la Marx. Nilipohusianisha kisa cha kaptura kubwa ya dogo anayeweka kidole mdomoni na visa vya Kaptura la Marx nilijikuta ninaangua kicheko. Ni kicheko ambacho kinatangulia tafakuri. Kwa hakika, baada ya kicheko, kinachofuatia ni huzuni. Ni huzuni ndiyo!
Katika tamthilia hiyo, Prof. Kezilahabi anaonesha kwamba baada ya uhuru wa nchi nyingi za Afrika, baadhi ya viongozi wa bara hili walikopa na kuiga itikadi na mifumo ya kigeni bila kuielewa vizuri namna ya kuitekeleza. Viongozi hao walijikuta wanasafiri weee bila kufanikiwa na hatimaye kuwasababishia maisha magumu wananchi wao. Wanasema, asiyejua anakoelekea, hapotei. Kinyume chake, ukiona mtu anasema kwamba amepotea njia, maana yake anajua alikuwa anaelekea wapi. Hali hii ni tofauti na watawala wanaozungumziwa katika tamthilia hii. Watawala hawa, wala hata hawajui k**a wamepotea bali huendelea husukumiza mbele wananchi na kuwaswaga k**a mbuzi ili waende nao. Shida kubwa, kwa mujibu wa tamthilia hii, ni watawala wa Kiafrika kutokaa chini na kutafakari kwa kina, ni itikadi na mifumo ipi ambayo ni mwafaka kwa Waafrika katika mazingira yao wenyewe. Huku ndio kucheza ngoja ya jirani kikasuku au kuvaa kaptura za watu hata k**a hazituenei. Kwa kuwa siasa si uwanja wangu, ngoja niishie hapo kuhusu tamthilia ya Kaptura la Marx.
Pamoja na kwamba nimeachana na mambo ya watawala, basi mimi na wewe tujikague k**a nasi tumevaa kaptura ambazo ni zetu na zinatuenea. Ngoja nianze kwa kukugeukia kidogo: Swali la kwanza, hiyo kaptura yako uliyovaa una uhakika ni yako kweli? Swali la pili, kaptura hiyo inakuenea? Twende na maswali hayo na ninakuhakikishia kwamba kwa wiki hii walau yanatutosha.
Katika kutafakari namna tunavyoishi, nimekumbuka stori za kijiweni. Ninasema ni za kijiweni kwa sababu sina uhakika sana k**a ni za kweli. Nikiwa kijiweni nilikutana na stori ambazo wewe na mimi tunaweza kuzitafakari na kuona k**a zina ukweli au la.
Katika stori ya kwanza, jamaa mmoja alipomaliza chuo, alipata ajira serikalini. Kwa mwezi, jamaa alikuwa analipwa S*T. 1,200,000/= baada ya makato yote. Kabla ya ajira, jamaa alikuwa na ndoto ya kununua gari zuri aina ya BMW katika maisha yake. Alisononeka sana alipokuwa anaona watu mitaani wanamtimulia vumbi na magari hayo mazuri. Akasema, siku Mungu akimjalia, ipo siku naye atawakomesha. Mara tu alipoajiriwa na kugundua kwamba kuna fursa ya kukopa kwa miaka 9, haraka alienda kukopa benki na akanunua BMW yake fasta. Gari lile lilimtesa sana kwani alishindwa kumudu gharama za mafuta na matengenezo yake. Maisha yake yakawa magumu sana kwa sababu, mkopo ule ulimfanya hata kula yake iwe duni. Alianza kuwaza kwamba huenda kuna mtu kamroga asiendelee k**a wengine mitaani. Huyu unadhani kaptura aliyokimbilia kuvaa ilikuwa yake! Je, ilimwenea! Angalia jinsi alivyoishia kutembea kila siku akiishikilia isidondoke. Huyu, k**a yule dogo tu bwana! Usicheze na kaptura za watu aisee!
Katika stori ya pili, kuna jamaa mwingine alipomaliza masomo ya chuo kikuu na kuona ajira hazieleweki, aliamua kufanya tathmini ya kibiashara katika eneo analoishi. Alibaini kwamba eneo lile lilihitaji huduma ya duka la mazao. Hivyo, aliomba mtaji kidogo kwa ndugu na akafungua duka. Alikuwa ananunua mazao mikoani na kuweka dukani kwake. Alianza kidogo na taratibu akakua, duka likawa kubwa sana. Wateja walizoea duka lile na jamaa akawa ametoka kimaisha.
Baada ya muda mrefu kidogo, kijana mwenzake aliyemaliza naye chuo alimtembelea na kuona hatua aliyopiga. Alimuonea wivu sana rafiki yake kwa mafanikio yale. Katika kuongea na watu wa pale, kijana akaambiwa kwamba kuna fremu ya biashara jirani na pale, inapangishwa. Naye, kwa haraka akatafuta kitu cha kuweka dhamana, akakopa fedha benki. Alifungua duka la nafaka pembeni ili amnyang'anye wateja rafiki yake. Kitu cha kushangaza, duka lake halikuchanganya. Lilikuwa halikui kwa sababu ya kukosa wateja. Mwishowe, alifunga duka na kumchukia rafiki yake na akaanza kusema kwamba rafiki yake ni mshirikina na mfuasi wa Freemasons. Unadhani huyu alikosea wapi? Kaptura aliyokimbilia kushona ilikuwa yake?
Mpendwa msomaji wangu, mimi na wewe nasi tuna kaptura zetu. Hizi ni zetu kweli na zinatuenea? Katika safari ya tafakuri hii, wala usipotee njia. Ninachokuambia tu ni kwamba kabla ya kufanya au kutekeleza mikakati yetu, tufanye utafiti, tufanye tathmini kisha tuvae hizo kaptura zetu. Tusipofanya hivyo, maendeleo tutaendelea kuyasikia kwa watu. Kila mara tutakuwa tukipambana na kaptura zetu zisizotuenea ambazo mara zote zinataka kudondoka. Kwa sababu ya kuvamia kaptura za watu ndiyo maana tuna wanamuziki wasiovutia, waandishi wa vitabu visivyo na mvuto, walimu wa ovyo, madereva wa ovyo, wanasiasa wachumiatumbo, kwa kutaja wachache tu. Sasa na wewe usiniulize kuhusu kaptura yako. Itafute kisha pima k**a inakuenea au la! Kila la heri.
Tukutane tena Jumatatu ijayo. Asante sana kwa kusoma makala yangu.
=============
©️ Leonard Bakize, 2025
Mwalimu wa uandishi, mwandishi, mhariri, mfasiri na mchapishaji
26.05.2025
+255 755 643 590
[email protected]
********