13/08/2026
Sillo Azindua Miradi ya Maendeleo yenye Thamani ya Zaidi ya Milioni 370 Babati Vijijini
Naibu Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Mbunge wa Jimbo la Babati Vijijini, Daniel Sillo, amezindua miradi mbalimbali ya maendeleo katika Kata ya Arri, wilayani Babati, ikiwemo vyoo katika Shule za Msingi Arri na Endasago pamoja na Jengo la Wazazi katika Zahanati ya Kijiji cha Ariitsaayo.
Miradi hiyo imejengwa kwa ushirikiano kati ya wananchi na Karim Foundation International, ikiwa ni sehemu ya juhudi za kuboresha huduma za elimu na afya katika maeneo ya vijijini.
Kwa mujibu wa taarifa zilizotolewa, miradi hiyo imegharimu zaidi ya Shilingi milioni 370, ambapo Shule ya Msingi Endasago imetumia Shilingi milioni 118.297, Shule ya Msingi Arri takribani Shilingi milioni 129, huku Jengo la Wazazi katika Zahanati ya Ariitsaayo likigharimu Shilingi milioni 123.
Akizungumza wakati wa uzinduzi wa miradi hiyo, Sillo ameipongeza Serikali kwa kuweka mazingira wezeshi yanayowavutia wadau mbalimbali wa maendeleo kushirikiana na Serikali katika kuwekeza kwenye sekta muhimu zikiwemo elimu na afya.
Amesema ushirikiano kati ya Serikali, wananchi na mashirika ya maendeleo ni muhimu katika kuongeza kasi ya utekelezaji wa miradi na kuboresha huduma zinazotolewa kwa wananchi.
Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkazi wa Karim Foundation International, Shau Erro, amesema shirika hilo litaendelea kushirikiana na Serikali katika kutekeleza miradi mbalimbali ya maendeleo na kuunga mkono utekelezaji wa Ilani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM).
Naye Diwani wa Kata ya Arri, Paul Masong, amelishukuru Karim Foundation International kwa kuendelea kushirikiana na wananchi na kujenga miradi hiyo muhimu katika Kata ya Arri, akisema miradi hiyo itasaidia kuboresha huduma za kijamii kwa wananchi.