04/09/2026
*KANUNI KUU 20 ZA RSA TANZANIA, (Toleo la 2022)*
Katika majadiliano yoyote yanayoendeshwa katika majukwaa ya RSA, yawe ya mtandaoni au ya nje ya mtandao, kila RSA atazingatia kanuni na miongozo ifuatayo:
1. *HABARI SAHIHI:*
Hairuhusiwi kuandika habari yoyote isiyo ya ukweli ama ya kufikirika tu na kuipa uhai kuwa ya kweli.
2. *UHAKIKA WA TAARIFA*:
Thibitisha taarifa kabla hujaituma na k**a huna uhakika sema “sent as received, for verification”au “Habari hii Haijathibitishwa”. Hapa utaeleweka kuwa unataka jambo lifuatiliwe kujua ukweli wake na kwamba wewe si chanzo halisi cha taarifa.
3. *UKAMILIFU WA TAARIFA:*
Ripoti tukio kwa kutoa taarifa inayojitosheleza kwa kutaja nani muhusika (jina/namba ya gari/uelekeo), nini kimetokea, wapi limetokea, na ungependa nini kifanyike.
4. *HABARI ZILIZOKATAZWA*:
Ni marufuku kupost habari zinazohusu siasa, vichekesho, matangazo ya kibiashara, michezo, muziki, sticker, dini au habari binafsi labda k**a zimetokea barabarani mf.ajali, homa, kuibiwa, breakdown, na kubambikiwa kosa/jinai. K**a huna hakika na habari tafadhali, mtumie admin inbox kwanza.
5. *KUHUSU SALAMU*:
Unapoingia kundini kila siku kwa mara ya kwanza, unaruhusiwa kutoa salamu na kisha kuendelea kutoa habari. Mf. Habari za asbh rsa, njia ya makongo iko shwari, au hapa Arusha kuna jamm maeneo ya sekela.
6. *TAARIFA ZA KIPAUMBELE*:
Taarifa tunazozipa kipaumbele hapa ni zinazohusu msongamano wa magari ili kuwasaidia TCC kujua kwa kuelekeza nguvu kazi; ajali; ukiukaji sheria barabarani; utendaji mbovu wa askari. Aidha UKIMYA wa muda mrefu bila kutoa taarifa au kuchangia mada kwa mwezi mmoja na Zaidi hautavumilika. Aidha, taarifa za kitaifa na zile za kuelimisha kutoka serikali ambazo umma unapaswa kuzijua zitapewa kipaumbele hata k**a hazihusiani moja kwa moja na usalama barabarani.Admins watachagua taarifa hizo na kuzileta kwenye groups.
7. *UUNGAJI WA WANACHAMA*: Huruhusiwi kumwongeza mjumbe yeyote bila ruhusa ya admin na bila kwanza kumwelezea huyo mjumbe mpya nini kinachofanyika hapa rsa. Aidha mtu anayemwombea mtu mwingine uanachama ni sharti ahakikishe anampa mtu huyo kanuni na azikubali, ikiwemo kuandika jina angalau moja kwenye profile yake na kuweka picha ya utambulisho. Aidha amweleze kuhusu wajibu wake wa kuwa active, na kuzingatia kanuni.
8. *WAJIBU WA RSA*:
Kuwa RSA ni kuwa mstari wa mbele katika kutii sheria za barabarani; kukiri kosa na kulipa faini au kuomba radhi; kujitolea; kutoa taarifa za barabarani; kujielimisha na kuwaelimisha wengine. RSA hayuko hapa ili kuwa juu ya sheria au kuwa uchochoro wa kuombea feva bila kuwajibika, pia usitake attention ambazo si za lazima.
9. *PICHA*:
Hairuhusiwi kuweka picha mbaya za ajali zisizowastahi marehemu. Picha yoyote unayoweka humu au video sharti iwe ina maelezo yanayojitosheleza kuelimisha au kuchukua hatua. Pia si ruksa kurudia rudia mara nyingi kutuma picha hizo hizo au zinazotoa ujumbe mmoja iwapo ulizotoa awali zinajitosheleza.
10. *KAULI/LUGHA YA MAWASILIANO*:
Lugha ya Matusi, vijembe, siasa hairuhusiwi katika foram za RSA, wala ubishi usio wa hoja. Siku zote usinungúnike, lalamika kwa kutoa hoja na ikiwezekana pendekeza suluhisho.
11. *TRAFIKI JAMII*:
RSA sio Polisi wala jasusi yeye ni trafiki jamii na ataendelea kuwa trafiki jamii kazi kubwa ni kutii sheria, kujielimisha na kuelimisha, na kutoa taarifa na kuchochea mabadiliko. Hatuhitaji shujaa mfu (dead hero), usihatarishe maisha yako au usalama wako kwa kupiga picha au kushughulika na tatizo/suala lililo nje ya uwezo wako. Toa taarifa tu.
12. *UONGOZI*:
Rsa inaongozwa kwa sheria na kanuni. Ni marufuku kujiamulia mambo bila kupata Baraka za uongozi yaani Mwenyekiti, Katibu, Mlezi au Admins. Na kwa upande wa matawi ya RSA mikoani, kila tawi litazingatia mamlaka yaliyo kwenye himaya yake na kuheshimu mamlaka ya taifa.
13. *RUFAA/MALALAMIKO*:
Ikiwa utaona umeonewa iwe kwa kufungiwa au kukanywa basi unaruhusiwa kulalamika kupitia mmoja wa wanachama ili alifikishe barazani watu waweze kujadili. Vivyo hivyo ukifungiwa unaweza kupitia mjumbe mmoja wapo au admins kuomba msamaha na kuandika ujumbe wa kuomba kurejeshwa kundini, na kwa masharti utakayopewa.
14. *MAAMUZI YA ADMINS*:
Wakati wowote na wanapoona inafaa admins wanaweza kuchukua hatua yoyote kwa mwanachama atakayekiuka utaratibu. Hatua zinaweza kuwa onyo, karipio, au kusimamishwa kwa muda. Admins hawaruhusiwi kutofautiana hadharani isipokuwa inbox.
15. *SIRI/USALITI*:
kila rsa ana wajibu wa kutunza siri za kundi zinazohusiana na taarifa za uvunjifu wa sheria barabarani. Kumtaja mtoa taarifa au kuvujisha utambulisho wake kwa mkosaji ni kosa na ni usaliti na yeyote atakayefanya hivyo hatua kali zitachukuliwa dhidi yake.
16. *VITISHO*:
ni marufuku rsa yeyote kujaribu ama kumtisha mwenzake inbox au kwa sms au kwa simu au njia nyingine yeyote ila kwa sababu tu ya jambo alilolisema au taarifa aliyoitoa humu inapoenda kinyume na maslahi ya mtishaji au mtuhumiwa.
17. *MARUFUKU*:
Ni marufuku kwa RSA yeyoye kutumia Uanachama wake kwaajili ya kulinda maslahi yake binafsi, kutisha, kudhoofisha juhudi za RSA, kupotosha, kutotii sheria, kuomba upendeleo maalumu, kudhalilisha au kuhujumu juhudi zozote za RSA.Kufanya hivyo ni kosa na hatua za kinidhamu zitachukuliwa mara moja.
18. *UTII WA SHERIA*:
Kila RSA atawajibika kikanuni na kisheria kutii sheria za barabarani kwa yeye kuwa mfano wa kuigwa na mwingine. Mathalani pale atakapopigwa faini kwa kosa halali alilolitenda, hatakiwi kubisha bali kulipa, na pale atakapokuwa amesingiziwa kosa ambalo hajalitenda au halieleweki basi ataomba ufafanuzi ngazi kwa ngazi au kutoa taarifa kwa uongozi wa RSA ilia pate kushauriwa na kusaidiwa.
19. *MAHUSIANO MEMA*:
Siku zote RSA wataishi, kuhusiana na kuheshimiana k**a familia, watakuwa tayari kusaidiana na kushirikishana mambo mbalimbali ya kimaendeleo, ya kihuzuni na kifuraha. Endapo RSA anasafiri kwenda mkoa wowote au sehemu yoyote nchini, atajitahidi kuwaarifu na kuwatafuta RSA waliopo eneo analokwenda ili kukuza mahusiano mema na kubadilishana mawazo.
20. *ADHABU*:
Mtu yeyote akakayekiuka kanuni hizi, kulingana na ukubwa wa kosa, anaweza kusimamishwa jukwaani au kwenye mjadala mara moja na kupelekwa kwenye k**ati ya nidhamu ambako suala lake litajadiliwa na kutolewa maamuzi. Utaratibu huu utawahusu wanachama wanaotumia mitandao ya telegram na whatsapp na mwingine wowote unaofanana na huo, kwa wale wa facebook wanaweza kuondolewa moja kwa moja baada ya kupewa onyo na kutotii. Mtu yeyote atakayesaliti harakati za RSA atashughulikiwa kinidhamu na adhabu yake inaweza kuwa kufutwa uanachama au kusimamishwa kwa kipindi Fulani.
*KILA BALOZI ANA WAJIBU WA KUSOMA NA KUZIELEWA KANUNI HIZI KISHA KUZIFUATA KWA BIDII ZOTE*