07/05/2026
TWCC YAONGOZA WANAWAKE KUCHANGAMKIA FURSA JUKWAA LA BIASHARA TANZANIA NA KENYA
Tarehe 4, Mei 2026
DAR ES SALAAM:
Rais wa Chemba ya Wanawake Wafanyabiashara Biashara Tanzania TWCC, CPA Mercy Silla, amewaongoza wanawake wajasiriamali nchini kushiriki Kongamano la Biashara kati ya Tanzania na Kenya, lililofanyika tarehe 4 Mei 2026 katika ukumbi wa JNICC, Dar es Salaam.
Kongamano hilo lililobeba kaulimbiu ya "Kufungua Ukuaji wa Sekta Binafsi na Uwekezaji," lilikusanya wadau wa kibiashara na viongozi wa kitaifa kutoka Tanzania na Kenya kwa lengo la kujadili fursa za biashara na uwekezaji.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, akizungumza katika kongamano hilo, alikumbusha kuwa ushirikiano wa kiuchumi kati ya mataifa haya mawili ni muhimu zaidi kuliko ushindani usio na manufaa. Kwa upande wake, Rais wa Kenya, Mhe. Dkt. William Ruto, alisisitiza kuwa nchi hizi zina uwezo wa kukuza thamani ya biashara kufikia dola bilioni moja zikifanya kazi k**a mfumo mmoja. Viongozi wote wawili walibainisha kuwa sekta binafsi ndiyo mhimili mkuu wa kukuza uchumi katika nchi hizi mbili.
Katika hatua nyingine, kupitia kongamano hili imehimizwa uimarishaji wa miundombinu ya nishati, mawasiliano, na sera za kodi zinazotabirika ili kurahisisha ufanyaji biashara.
Katika kuelekea utekelezaji wa vitendo, kongamano hilo limefungua ukurasa mpya kwa kuoanisha mifumo ya ukaguzi wa ubora kupitia mashirika ya TBS na KEBS, pamoja na kuanzisha Baraza la Biashara la Pamoja. Miradi ya kimkakati, ukiwemo ujenzi wa bomba la gesi kuelekea Mombasa na kuunganisha reli ya kisasa (SGR), ilitajwa k**a vipaumbele vya kuchochea kasi ya uchumi.
Aidha, washiriki walishuhudia kusainiwa kwa Tamko la Pamoja la Makubaliano (Joint Communique) na mikataba ya ushirikiano kati ya Taasisi mbalimbali za uwezeshaji biashara kutoka Tanzania na Kenya. Mikataba hiyo inaweka mkakati madhubuti wa kuongeza ushindani wa bidhaa za Kitanzania nchini Kenya na kanda nzima ya Afrika Mashariki, huku ikipunguza gharama za mawasiliano kupitia mfumo wa "One Network Area."