04/06/2026
Mapema wiki hii Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC) kilishiriki mhadhara wa umma ulioandaliwa na Chuo Kikuu Mzumbe, Ndaki ya Dar es Salaam, uliolenga kuongeza uelewa wa wanafunzi kuhusu nafasi ya haki za binadamu katika maendeleo ya kijamii na kiuchumi.
Katika mhadhara huo ulioongozwa na mada isemayo “Haki, Biashara na Huduma: Mtazamo wa Haki za Binadamu katika Utoaji wa Huduma za Kijamii na Kiuchumi Tanzania,” LHRC iliwakilishwa na Afisa wa Haki za Binadamu na Biashara, Bw. Clay Mwaifwani, ambaye aliwasilisha mada na kuongoza majadiliano kuhusu umuhimu wa kuzingatia haki za binadamu katika utoaji wa huduma za kijamii na utekelezaji wa shughuli za kiuchumi.
Akizungumza wakati wa mhadhara huo, Mwaifwani alieleza kuwa maendeleo ya kiuchumi yanapaswa kuzingatia haki za binadamu ili kuhakikisha kuwa wananchi wote wananufaika kwa usawa huku akisisitiza juu ya wajibu taasisi za umma na binafsi kuzingatia misingi ya uwajibikaji, ushirikishwaji na usawa katika utoaji wa huduma na utekelezaji wa mipango ya maendeleo.
Hatahivyo, Mwaifwani aliwahimiza wanafunzi kutumia elimu na maarifa wanayoyapata chuoni kuchangia maendeleo ya jamii kwa kuzingatia misingi ya haki, maadili na uwajibikaji, akibainisha kuwa vijana wana nafasi muhimu katika kuhamasisha na kutetea haki za binadamu kupitia taaluma na ushiriki wao katika shughuli mbalimbali za kijamii na kiuchumi.
Kupitia ushirikiano na taasisi za elimu ya juu, LHRC inaendelea kuhamasisha mijadala kuhusu haki za binadamu na biashara, na uwajibikaji wa wawekezaji pamoja na ulinzi wa walaji wa bidhaa na hudumakwa maendeleo jumuishi na endelevu.