02/05/2026
CHUNYA TUMEJIANDAA KULETA MAENDELEO KATIKA SEKTA ZOTE - MH MASACHE
Mbunge wa Jimbo la Lupa-Chunya, Mheshimiwa Masache N. Kasaka, amesema Chunya imejipanga kuleta maendeleo katika sekta zote kwa kushirikiana na wadau mbalimbali, hususan wachimbaji wa madini ambao ni nguzo muhimu ya uchumi wa eneo hilo.
Akizungumza alipokuwa mgeni rasmi katika kongamano lililoandaliwa na Green Mining Awareness, Mheshimiwa Masache amesema serikali imeendelea kuweka mazingira wezeshi yanayorahisisha shughuli za uchimbaji, hatua inayochochea ukuaji wa uchumi na kuboresha maisha ya wananchi.
Katika kongamano hilo, wachimbaji pamoja na taasisi mbalimbali waliishukuru serikali kwa jitihada hizo, huku wakieleza changamoto zinazowakabili katika shughuli zao za kila siku. Mheshimiwa Masache aliahidi kuzibeba changamoto hizo na kuziwasilisha bungeni ili zipatiwe ufumbuzi wa kudumu.
Katika tukio hilo, Mheshimiwa Masache aliambatana na viongozi mbalimbali akiwemo Mkuu wa Wilaya ya Chunya, Mheshimiwa Batenga; Katibu Tawala Wilaya, Ndugu Anakleth Michombero; Mwenyekiti wa Halmashauri ya Chunya, Mheshimiwa Kelvin Nshishi; Diwani wa Kata ya Matundasi, Mheshimiwa Alphonce Maganga; Katibu wa CCM Wilaya, Ndugu Jockery Seleman; pamoja na Mwenyekiti wa Wanawake Wilaya Chunya, Ndugu Ezelina Mwakisole.