16/01/2026
https://www.facebook.com/photo?fbid=122113408659139992&set=a.122113409379139992
Asasi ya Maendeleo ya Jamii na Mabadiliko (CDTF NGO) kwa kushirikiana na watalaamu wa Halmashauri ya Mlimba walihamasisha wanakijiji wa Kijiji cha Tanganyika, kata ya Masagati, wilaya ya Mlimba, Mkoa wa Morogoro kuhusu utunzaji mazingira na ufugaji nyuki ili kutoa fursa kwa vijana wengi kukuza kipato chao kupitia shughuli endelevu zinazolinda mazingira.
Wananchi wakiwemo wakulima, wafugaji wa nyuki, vijana, wanawake, Viongozi wa Serikali ya Mtaa na Kata, pamoja na wadau mbalimbali walihudhuria na walipata fursa ya kujifunza kuhusu umuhimu wa utunzaji mazingira na ufugaji nyuki.Uhamasishaji ulilenga kuwaandaa wananchi hasa vijana kujihusisha na shughuli endelevu za kuwapatia kipato huku wakilinda misitu na mazingira.
Akizungumza na Wanakikijiji waliohudhuria katika Mkutano huo Bw. Justine Chaki, Afisa Ufugaji Nyuki Kata ya Masagati aliwahimiza kutumia mbinu bora za ufugaji nyuki ikiwemo matumizi ya mizinga yenye tija, usimamizi wa mizinga na uvunaji. Aliongeza kuwa ubora wa mazao ya nyuki unatakiwa kuzingatia uvunaji, uchakataji na uhifadhi wake.
Nae Bw. Sakumi Mwikwabe, Afisa Maendeleo ya Jamii Kata ya Masagati alihimiza wananchi hasa vijana kujiunga kwenye vikundi ili iwe rahisi kutekeleza miradi yao kwa ushirikiano. Aliomba CDTF NGO kutoa mafunzo ya kina ili yawasaidie kufuga, kutafuta masoko ya uhakika wa bidhaa zao.
Bi. Letisia Matikila Mkazi wa Kijiji cha Tanganyika alishukuru elimu aliyoipata iliyowatia hamasa ya kutunza mazingira na kushiriki kwenye vikundi kufuga nyuki. Alianisha changamoto waliyokuwa nayo ni mtaji na masoko katika sekta ya ufugaji nyuki.
Asasi ya Maendeleo ya Jamii na Mabadiliko (CDTF NGO) inafanya kazi na Jamii kubadilisha maisha yao yawe bora. Asasi ilianzishwa mwaka 2005 chini ya Community Development Trust Fund na ilihuisha usajili wake mwaka 2023. Bw. Stanford Kalala, Mkurugenzi Mtendaji wa CDTF NGO alisema asasi inaendelea kuhamasisha rasilimali kutoka kwa wadau wa maendeleo ili kuwezesha vijana washiriki katika maendeleo ya jamii na kubadili maisha yao yawe bora. Kwa sasa asasi unafadhiliwa na Taasisi ya Maendeleo ya Jamii.