04/04/2026
MBUNGE KIGAMBONI AAHIDI KUIMARISHA USHIRIKIANO NA KUBORESHA USTAWI WA MAAFISA USAFIRISHAJI
Mbunge wa Jimbo la Kigamboni, Mhe. Haran Sanga ameahidi kuimarisha ushirikiano na maafisa usafirishaji kwa kufanya ziara za “mgundi kwa mgundi” ili kusikiliza na kutatua kero zao, hatua inayolenga kuongeza ufanisi wa kazi, kuimarisha usalama na kuboresha ustawi wa madereva wa pikipiki.
Akizungumza na maafisa usafirishaji wa Chama cha Madereva na Wamiliki wa Pikipiki Mkoa wa Dar es Salaam (CMPD) katika mkutano uliofanyika Kigamboni, Jijini Dar es Salaam, Mhe. Sanga amesisitiza umuhimu wa kufanya kazi kwa kuzingatia sheria na kuepuka kujichukulia sheria mkononi, huku akihimiza ushirikiano katika masuala ya usalama.
Aidha, katika kuimarisha hali ya kifedha ya Maafisa Usafirishaji, ameagiza kuanzishwa kwa SACCOS ya chama hicho na kuchangia kiasi cha shilingi laki tano kwa ajili ya kufungua akaunti, hatua itakayowawezesha madereva kupata mikopo na huduma za kifedha kwa urahisi.
Sambamba na hilo, Mbunge huyo ametoa udhamini wa pikipiki za mkopo akishirikiana na kampuni ya ENERSCI LTD huku pia akiahidi kugharamia mafunzo ya udereva na leseni kwa viongozi wa maafisa usafirishaji ili kuongeza ufanisi na usalama katika sekta hiyo.
Kwa upande wake, Mbunge huyo ameendelea kusisitiza dhamira yake ya kufanya kazi kwa karibu na makundi mbalimbali, ikiwemo maafisa usafirishaji, katika kusikiliza na kutatua changamoto zao kabla na baada ya kuchaguliwa kwake, jambo linaloonyesha kujali na uwajibikaji kwa wananchi wa Kigamboni.