12/06/2026
Mashujaa walipata nafasi ya kusikia mada mbali mbali katika mtoko wao:-
Ufuatiliaji wa Afya Baada ya Matibabu ya Saratani
Dkt. Sarah Nyagabona, Daktari Bingwa wa Saratani kutoka Hospitali ya Taifa Muhimbili, alisisitiza umuhimu wa ufuatiliaji wa afya mara kwa mara baada ya kumaliza matibabu ya saratani.
Washiriki walielimishwa kuhusu umuhimu wa kuhudhuria miadi za kliniki k**a ilivyopangwa, kufuata ushauri wa wataalamu wa afya, na kutambua mapema dalili zinazoweza kuashiria kurejea kwa ugonjwa. Pia walihamasishwa kuzingatia mtindo bora wa maisha ili kuimarisha afya, ustawi na ubora wa maisha baada ya matibabu.
Msaada wa Kisaikolojia na Kijamii katika Usimamizi wa Saratani
Safari ya saratani haiathiri mwili pekee, bali pia hisia, mahusiano na ustawi wa kiroho.
Kupitia mjadala huu, washiriki walipata nafasi ya kujibiwa maswali kuhusu changamoto za kihisia, kisaikolojia, kijamii na kiroho zinazoweza kujitokeza wakati na baada ya matibabu ya saratani.
Wataalamu walisisitiza umuhimu wa ushauri nasaha, msaada wa familia, vikundi vya usaidizi vya mashujaa wa saratani (Cancer Support Groups), pamoja na huduma za afya ya akili katika kuwasaidia wagonjwa na mashujaa kuendelea kuishi kwa matumaini, nguvu na ustawi.
Saratani na Lishe
Bi. Rebeca Lebi alitoa elimu na mwongozo wa vitendo kuhusu umuhimu wa lishe bora katika safari ya saratani na maisha baada ya matibabu.
Washiriki walijifunza namna ya kuchagua vyakula vyenye virutubisho muhimu, kudumisha lishe yenye uwiano sahihi, na kukabiliana na changamoto za lishe zinazoweza kujitokeza kutokana na matibabu ya saratani.
Lishe bora ni sehemu muhimu ya kuimarisha afya, kuongeza nguvu za mwili na kuboresha ustawi wa mashujaa wa saratani.
Afya bora huanza na uchaguzi bora wa chakula kila siku.