02/01/2025
Katibu Bakwata Wilaya ya Temeke awa Mgeni rasmi Mkutano Mkuu wa UWAMAA.
Katibu wa Bakwata Wilaya ya Temeke Ndugu Mudhihiri Mchoye amehudhuria katika Mkutano Mkuu wa Umoja wa Walimu wa Madrasa Kata ya Azimio (UWAMAA) uliofanyika siku ya Jumapili Desemba 29, 2024 katika ukumbi wa Idd Nyundo uliyopo Halmashauri ya Manispaa ya Temeke.
Akizungumza na Walimu hao Ndugu Mchoye amesema kuwa, Walimu wa Kata ya Azimio ni mfano wa kuigwa kwa Kata nyingine za Wilaya ya Temeke kwa kuanzisha Umoja huo.
Aidha, Ndugu Mchoye amewaasa viongozi wa Umoja kusimamia malengo ya kuanzishwa kwa Umoja huo ili kuleta tija kwa Mwalimu mmoja mmoja, Kata ya Azimio na Uislamu kwa ujumla.
Kadhalika, kutokana na wimbi kubwa liliojitokeza la baadhi ya vikundi kujinasibisha na madrasa na kuonekana vikifanya mambo yasiyofaa katika jamii yanayodhalilisha Waislamu na Uislamu, Katibu huyo ameutumia Mkutano Mkuu huo kuonya na kutoa maagizo kwa Madrasa zote zilizopo Kata ya Azimio kubaini na kuzichua Madrasa au vikundi vinavyofanya mambo hayo ambayo kimsingi yanachafua taswira njema ya Uislamu.
Katika Mkutano huo, Ndugu Mchoye amewahakikishia Walimu kuwa ofisi yake ipo wazi muda wote na ipo tayari kutoa ushirikiano katika jambo lolote ambalo watahitajia msaada.
Imeandaliwa na,
Issa Mpendu - Amiri Idara ya Habari na Mawasiliano, Juvikiba (W) Temeke.