02/09/2026
Msajili wa Hazina ateta na uongozi wa kampuni ya Barrick
Na Mwandishi wa OTR
Dar es Salaam. Msajili wa Hazina, Bw. Nehemiah Mchechu, amekutana na kufanya mazungumzo na wawakilishi wa Barrick Corporation, mwanahisa mwenza wa Twiga Minerals Corporation Limited (TWIGA), pamoja na uongozi wa TWIGA, kujadili maendeleo na masuala mbalimbali yanayohusu uendeshaji wa miradi inayosimamiwa na kampuni hiyo.
Mazungumzo hayo yalifanyika Jumanne, Septemba 1, 2026, wakati ujumbe wa Barrick ulipofanya ziara katika Ofisi ya Msajili wa Hazina (OTR), jijini Dar es Salaam.
Ujumbe wa Barrick uliongozwa na Roelie G*y Von Pittius, Meneja wa Fedha wa Barrick kwa Afrika na Mashariki ya Kati, akiambatana na Candace Simpson, Meneja wa Kodi wa Afrika na Mashariki ya Kati; Melkiory Ngido, Meneja wa Barrick nchini Tanzania; na Judith Chambua, Meneja wa Kodi wa Barrick Tanzania.
Katika kikao hicho, Serikali, kupitia OTR, na Barrick, ambao ni wanahisa wenza wa TWIGA, walijadili masuala mbalimbali yanayohusu maendeleo na uendeshaji wa miradi ya uchimbaji wa dhahabu inayomilikiwa kwa ubia kupitia TWIGA.
Miongoni mwa miradi iliyojadiliwa ni pamoja na migodi ya North Mara na Bulyanhulu, pamoja na Buzwagi, ambao kwa sasa upo katika hatua za mwisho za kufungwa.
Uongozi wa TWIGA pamoja na wataalamu kutoka Barrick walishiriki katika kikao hicho kwa kutoa taarifa na ufafanuzi kuhusu masuala mbalimbali yanayohusu maendeleo na uendeshaji wa miradi hiyo.
Akizungumza katika kikao hicho, Bw. Mchechu alisema Serikali, kupitia Ofisi ya Msajili wa Hazina, itaendelea kutoa ushirikiano unaohitajika katika kutatua changamoto mbalimbali zinazoweza kujitokeza katika uendeshaji wa miradi ya TWIGA, kwa lengo la kuhakikisha miradi hiyo inaendelea kwa ufanisi, kuongeza uzalishaji na kuchangia zaidi katika uchumi wa Taifa.
Aidha, Bw. Mchechu alisisitiza kuwa sekta ya madini inaendelea kuwa na mchango mkubwa katika uchumi wa Taifa na mapato ya Serikali, ikiwemo kupitia gawio linalotokana na uwekezaji wa Serikali katika kampuni za madini.
Bw. Mchechu alisema Serikali inathamini ushirikiano wake na Barrick na inaendelea kutumia uzoefu uliopatikana kupitia uhusiano huo katika kuimarisha sekta ya madini nchini.