06/05/2026
Tunapenda kutoa shukrani zetu za dhati kwa Deloitte Tanzania kwa imani, ushirikiano na uongozi madhubuti waliouonesha katika utekelezaji wa mradi wa Kizazi Hodari.
Tangu kuanzishwa kwa mradi huo, Deloitte Tanzania imekuwa mshirika muhimu katika kuhakikisha utekelezaji wenye ubora, uwajibikaji na matokeo yanayopimika. Kupitia ushirikiano huu, mradi umefanikiwa kufikia malengo yake kwa kiwango cha juu, ukiwa na mchango mkubwa katika kuboresha ustawi wa jamii, hususan kwa makundi yaliyo katika mazingira hatarishi katika mkoa wa Njombe.
Matokeo ya mradi huu yameacha alama chanya na endelevu, ikiwa ni pamoja na kuimarika kwa huduma za kijamii, kuongezeka kwa uelewa wa masuala ya maendeleo ya kijamii, pamoja na kuboreshwa kwa maisha ya walengwa kwa ujumla. Haya yote yanadhihirisha umuhimu wa ushirikiano kati ya taasisi za kiraia na sekta binafsi katika kusukuma ajenda ya maendeleo endelevu nchini.
Katika kuhitimisha mradi huo, baadhi ya viongozi wa Shirika la COCODA Tanzania pamoja na viongozi wa juu wa Deloitte Tanzania (Dorothy Matoyo na Kenneth Chima) walioongoza utekelezaji wa mradi wa Kizazi Hodari walionekana katika picha ya pamoja wakati wa hafla fupi ya kutamatisha mradi huo ngazi ya kanda, tukio lililoashiria mafanikio ya ushirikiano huo na dhamira ya kuendeleza juhudi za pamoja.
tunatambua na kuthamini mchango wa Deloitte Tanzania, na tunaamini kuwa ushirikiano huu utaendelea kuimarishwa zaidi ili kuongeza wigo wa athari chanya kwa jamii nyingi zaidi nchini.
Shirika linaendelea kujizatiti katika kubuni na kutekeleza mipango bunifu inayolenga kuleta maendeleo jumuishi na endelevu kwa Watanzania wote.