08/05/2026
CHADEMA PWANI WAUNGA MKONO MAAZIMIO YA KAMATI KUU ,YATAKA WALIOHUSIKA NA VURUGU ZA OKTOBA 29/2025 WACHUKULIWE HATUA
Na Gustaphu Haule,Pwani
CHAMA Cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) Mkoa wa Pwani kimeunga mkono maazimio 12 yaliyopitishwa na Kamati Kuu ya chama hicho na kutaka wale waliohusika na vurugu za Oktoba 29 wachukuliwe hatua za kisheria.
Maazimio hayo yameungwa mkono katika mkutano uliofanyika Mei 07/2026 katika Manispaa ya Kibaha kwa kuwashirikisha viongozi mbalimbali wa Jimbo na Wilaya wa Mkoa wa Pwani.
Katibu wa Chadema Mkoa wa Pwani Richard Mbalase amesema mbali na kuungana mkono maazimio ya k**ati kuu lakini pia mkutano huo umetumika kuwasilisha taarifa ya uchambuzi wa ripoti ya Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali ( CAG).
Mbalase amesema Kamati Kuu ya Chadema iliketi katika kikao chake Aprili 28 hadi Aprili 29/2026 ambapo katika kikao hicho walijadili na kupokea taarifa ya hali ya kisiasa nchini kuanzia Novemba 25/2025 hadi Aprili 24/2026.
Amesema Katika kikao hicho Kamati Kuu ya Chadema iliyokuwa ikiongozwa na Makamu Mwenyekiti John Heche imepitisha maazimio mbalimbali yanayopaswa kuungwa mkono na viongozi wote wa Tanzania Bara na Tanzania visiwani.
Mbalase, baadhi ya maazimio hayo ni kuhamasisha na kuomba umma wa Watanzania kusimama na wapenda haki kushirikiana na mwenyekiti wa Chadema Taifa Tundu Lissu ili kusudi aweze kuachiliwa bila masharti yoyote.
Amesema azimio lingine ni kutowatambua viongozi waliochaguliwa Oktoba 29/2025 kwakuwa hawakupata ridhaa ya Wananchi, kuwachukulia hatua wale wote waliohusika katika vurugu za Oktoba 29/2025,kuundwa kwa tume huru ya uchunguzi wa matukio ya vurugu ya Oktoba 29 na kuhakikisha familia zilizopoteza wapendwa wao wanalipwa fidia.
Maazimio mengine kuanzishwa kwa Katiba Mpya, kuanza rasmi kwa oparesheni ya mikutano ya hadhara ya kisiasa nchi nzima itakayojulikana kwa jina la Oparesheni Katiba Mpya,Free Tundu Lissu na kuwaongoza Wananchi kudai hatua za haraka za kupunguza bei ya mafuta.
Kwa upande wake mwenyekiti wa Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) Bumija Senkondo akiwasilisha taarifa ya uchambuzi wa ripoti ya CAG ametaka waliotajwa katika ripoti hiyo kuchukuliwa hatua mara moja.