01/06/2026
MSAJILI WA JUMUIYA ZA KIRAIA ATEMBELEA KITUO CHA MAENDELEO YA MTOTO NA KIJANA LONGIDO
Msajili wa Jumuiya za Kiraia nchini, Bw. Emmanuel Kihampa, leo ametembelea Kituo cha Maendeleo ya Mtoto na Kijana kinachosimamiwa na Kanisa la Baptist Longido mkoani Arusha kwa ushirikiano na Compassion International Tanzania (CIT).
Katika ziara hiyo, Bw. Kihampa alipata fursa ya kujionea na kusikiliza shughuli mbalimbali zinazolenga kumkomboa mtoto kutoka katika umasikini, zikiwemo mafunzo ya ujuzi wa mikono, vikundi vya kuweka na kukopa, huduma za afya, elimu, ulinzi wa mtoto na ustawi wa jamii kwa ujumla.
Viongozi wengine waliohudhuria ni pamoja na Mkurugenzi wa Compassion International Tanzania, Mary Lema, Askofu Mkuu wa Kanisa la Baptist Tanzania, Askofu Arnold Manase, viongozi na wataalamu wa serikali ngazi za kata na wilaya pamoja na wachungaji wa makanisa washirika wa CIT wilayani Longido.
Akizungumza baada ya kutembelea kituo hicho, Bw. Kihampa alilipongeza Shirika la Compassion International Tanzania na makanisa washirika kwa mchango wao katika maendeleo ya watoto na jamii.
“Nimefurahishwa na kazi kubwa inayofanywa hapa. Matokeo yanaonekana wazi kwa watoto, familia na jamii kwa ujumla. Nawapongeza Compassion International Tanzania na makanisa kwa juhudi hizi na ninawahimiza kuendelea kufanya kazi kwa ufanisi zaidi. Serikali itaendelea kushirikiana nanyi katika kuhakikisha watoto wetu wanapata fursa bora za kukua na kufikia ndoto zao,” amesema Bw. Kihampa.
Kwa sasa CIT inafanya kazi katika mikoa 22 na wilaya zaidi ya 90 huku zaidi ya watoto na vijana 125,000 wakihudumiwa kupitia vituo vya maendeleo ya mtoto na kijana zaidi ya 600.
.district_council